KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Monday, December 15, 2014

FIVE STARS MODERN TAARAB YAJA KIVINGINE, YAMNYAKUA SALHA, KUZINDUA ALBAMU MPYA DESEMBA 19 DAR

SALHA Aboud
MARYAM Aboud
MUSSA Kijoti
KIONGOZI wa Five Stars Modern Taarab, Ally J (kushoto)

MWIMBAJI nyota wa taarab nchini, Salha Abdul, amejiunga na kikundi cha taarab cha Five Stars kinachoongozwa na mpiga kinanda mahiri, Ally J.
Salha alitangaza uamuzi wake huo mwishoni mwa wiki kwa kile alichodai kuwa, umelenga zaidi kukuza kipaji chake.
Mwanadada huyo mwenye sura jamali na umbo lenye mvuto alisema amefikia uamuzi huo baada ya kushawishiwa kufanya hivyo na Ally J na pia baada ya kupata barakaa za mama yake mzazi.
"Nilipigiwa simu na Ally J akinieleza kwamba ana mazungumza na mimi na bila kusita nilimkubalia kwa sababu namheshimu sana,"alisema Salha, ambaye kabla ya kujiunga na Five Stars alikuwa kwenye kikundi cha Kings Modern Taarab.
Tayari Salma ameshaibuka na kibao kipya kinachokwenda kwa jina la Kishtobe, ambacho kimeshaanza kusikika kwenye vituo mbalimbali vya redio nchini.
Kwa mujibu wa Ally J, kikundi hicho kinatarajiwa kufanya uzinduzi wa albamu yake mpya Desemba 19 mwaka huu, utakaofanyika kwenye ukumbi wa Travertine, Dar es Salaam.
Ally J alisema kikundi chake kimeamua kutoka kivingine, ikiwa ni pamoja na kuboresha mipigo yake ya taarab kwa kuweka vionjo vipya kwa lengo la kuleta mvuto kwa mashabiki.
Aliwashukuru wadau mbalimbali wa taarab, ambao wameamua kukiongezea nguvu kikundi hicho ili kiweze kuwa tishio kama ilivyokuwa wakati kilipoanzishwa.
Five Stars ilipata pigo miaka miwili iliyopita baada ya wasanii wake 11 kufariki dunia katika ajali ya gari iliyotokea mkoani Morogoro.
All J alisema uzinduzi wa albamu ya kikundi hicho utapambwa na wasanii mbalimbali maarufu wa taarab nchini, wakiwemo wakongwe Khadija Omar Kopa, Mwanahawa Ally na Jokha Kassim.
Kwa upande wake, waimbaji Mussa Kijoti na Maryam Aboud walisema ujio wa albamu yao mpya utakuwa na kishindo kizito kwa vile wameamua kutoka kivingine.

No comments:

Post a Comment