KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Saturday, February 2, 2013

MUME WANGU ALININYANYASA SANA-SALHA



MWIMBAJI nyota wa kikundi cha taarab cha Dar Modern, Salha Abdalla
amesema moja ya sababu kubwa iliyomfanya aachane na mumewe ni wivu
wa kupindukia.
Akihojiwa katika kipindi cha Mitikisiko ya Pwani, kilichorushwa
hewani na kituo cha redio cha Times FM wiki hii, Salha alisema wivu
aliokuwa nao mumewe, ulisababisha aamini kila alichoelezwa, hata
kama ni cha uongo.
Akitoa mfano, alisema wakati aliposafiri na kikundi chake kwenda
mikoa ya kusini, mumewe alipelekewa maneno ya uongo kwamba alikuwa
na uhusiano wa kimapenzi na msanii mmoja wa kikundi hicho na
akaamini.
Anasema alishangaa wakati wakiwa kwenye ziara hiyo, mumewe alikuwa
akimpigia simu na kumuuliza iwapo amerudiana na kijana huyo, lakini
alikuwa akimkatalia katakata.
"Ni kweli huyo mwanaume alikuwa mpenzi wangi kabla sijaolewa,
lakini wakati tulipokuwa safarini, sikuwahi kuhusiana naye kwa
lolote. Isitoshe alikuwa ameshaoa nami nimeolewa,"alisema Salha.
Aliongeza kuwa, baada ya kurejea kutoka katika ziara yao, mumewe
akaanza kumfanyia vituko nyumbani, ikiwa ni pamoja na kutomuachia
pesa ya matumizi wala kuzungumza naye.
Anasema kila alipomuuliza kulikoni, mumewe alionekana kuwa na
hasira na kuondoka nyumbani alfajiri na kurudi usiku wa manane.
Salha anasema baada ya kuona maji yamemfika shingoni, aliamua
kutengana na mumewe, lakini jambo la kushangaza, wiki zake waliamua
kumpokonya vitu vyote vya nyumbani, hata alivyotunzwa kwenye
sherehe ya kitchen party.
Anasema mmoja wa wifi zake alikuwa akiwapigia simu shoga zake
kuwauliza vitu walivyomtunza wifi yake na alipotajiwa, alimtaka
Salma aviache.
Kwa mujibu wa Salha, kilichokuja kumshtua zaidi ni kuona mumewe
akianzisha uhusiano wa kimapenzi na binamu yake wa kike, ambao hata
hivyo alisema ulidumu kwa siku chache.
"Kuna wakati alinifuata na kuniomba turudiane, lakini nilimkatalia
kwa sababu alishanidhalilisha sana, ikiwa ni pamoja na kunitoa
magazetini, hivyo nisingeweza kurudiana naye,"alisema Salha.
Mwanadada huyo, ambaye kwa sasa anatamba kwa kibao chake cha
Ninauvua ushoga, alisema kwa sasa anaye mpenzi mwingine na
wanatarajia kufunga ndoa hivi karibuni.

No comments:

Post a Comment