KWA HABARI ZA MUZIKI WA TAARAB, WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL ramozaone@gmail.com

Saturday, August 11, 2012

DIDA: MTANGAZAJI WA REDIO ALIYEJITOSA KWENYE TAARAB


JINA la Khadija Shaibu 'Dida' si jina geni kwenye masikio ya mashabiki wa muziki wa taarab, hasa wanaosikiliza vipindi vya muziki huo kupitia kwenye vituo mbalimbali vya radio nchini.
Ni mtangazaji maarufu na mwenye mbwembwe nyingi kila anapotangaza kipindi cha muziki huo kupitia kituo cha radio cha Times FM. Na sasa ameamua kuwa mwimbaji wa muziki huo, ambao ulianza kumvutia tangu akiwa mdogo.
Umaarufu wa Dida, mama wa mtoto mmoja, mwenye umbo dogo,lugha ya tashtiti na yenye mvuto wa aina yake, tayari ameshaipua kibao kimoja cha muziki huo kinachojulikana kwa jina la ‘Waniache miaka 800’.
Dida alikizindua kibao hicho mwishoni mwa wiki iliyopita katika onyesho lililofanyika kwenye ukumbi wa hoteli ya Travertine iliyopo Magomeni, Dar es Salaam, akisindikizwa na kundi maarufu la muziki huo la Jahazi.
Akizungumza na mwandishi wa makala hii hivi karibuni mjini Dar es Salaam, Dida alisema ameamua kujitosa kwenye muziki huo kutokana na mapenzi makubwa aliyonayo katika fani hiyo.
"Huwezi kuamini, katika utoto wangu nilikuwa sipendi kabisa taarab na ilikuwa haiko kwenye damu, lakini baada ya kuwa mtangazaji, hasa wa kipindi cha taarab, nimetokea kuupenda tu,”alisema Dida.
"Nimeona kwa vile nimepata uzoefu wa kutosha kutokana na kuutangaza kwa muda mrefu muziki huo, nami niachie tungo yangu ili kujipima uwezo wangu," aliongeza.
Awali, Dida alipanga kumshirikisha kiongozi wa kundi la Jahazi, Mzee Yusuph katika kuimba wimbo huo, lakini mpango huo ulikufa kimya kimya na kuamua kuuimba yeye mwenyewe.
"Nilitaka kumshirikisha Mzee Yusuph kwa sababu bila ya unafiki,yeye yupo juu kwa sasa. Pia ndiye aliyenishauri mambo mengi hadi nikafanikisha kutunga wimbo huo," alisema.
Dida alisema anaamini wimbo huo utafanya vizuri na unaweza kuwa wimbo bora wa mwaka wa taarab.Mtangazaji huyo alijigamba kuwa, wimbo huo umesheheni vionjo vingi na siku ya uzinduzi alisindikizwa na kundi zima la Jahazi linalotamba na albamu yao ya sita ya 'My Valentine'.
Akizungumzia kazi yake ya utangazaji, Dida alisema kwake ni kipaji alichojaliwa kuwa nacho na Mwenyezi Mungu na alibaini kuwa nacho baada ya kumaliza masomo ya sekondari.
"Utangazaji kwangu ni kipaji nilichokipata ukubwani, nakumbuka nilipokuwa mdogo, sikuwa na kipaji chochote, hata mimi nashangaa, sielewi ilikuwaje," alisema.
Amemtaja mmoja wa watangazaji waliomvutia na kumfanya ajitose katika fani huyo kuwa ni marehemu Amina Chifupa 'Mpakanjia', aliyejizolea umaarufu mkubwa enzi za uhai wake kupitia kituo cha radio cha Clouds.
Kupitia kazi yake hiyo, Dida alisema amejikuta akipata maadui wengi, hasa wanawake wanaodhani kuwa anawapiga vijimbe anapokuwa akiendesha kipindi chake.Alisema baadhi ya wanawake hao humuandama kwa matusi kwa kumtumia ujumbe mfupi wa maneno kupitia simu yake ya mkononi, ambao anakiri kuwa, mara nyingi humuathiri kisaikolojia.
"Usione hivi, navumilia mambo mengi, tangu nianze kutangaza, nimejikusanyia maadui kibao, wengi ni wanawake wenzangu, lakini hiyo ni changamoto kwangu na nitazidi kusonga mbele," alisema.
Dida alisema maneno yake wakati anapotangaza kipindi cha mipasho hayalengi kumchafua mtu ama kumpiga vijembe yeyote, isipokuwa ni katika kukiboresha na kuwapa burudani wasikilizaji wake.
Mwanamipasho huyo amelitaja tukio ambalo hawezi kulisahau katika maisha yake kuwa ni la kuvumishiwa kuwa anajihusisha na dawa za kulevya, jambo ambalo amekana katakata kuhusika nalo.
"Siwezi kuusahau uvumi huo katika maisha yangu kwa sababu ulilenga kunichafua, lakini yote namuachia Mungu, najua atawabainisha wote walionienezea uvumi huo," alisema.
Amewaasa waimbaji chipukizi wa taarab nchini kuwa, watunge nyimbo zenye maadili na zenye kuleta ujumbe kwa jamii na waachane na majungu ili waweze kusonga mbele.
Amewashauri pia watangazaji wenzake, wawe na ushirikiano , wapendane na wasitupiane vijembe visivyo na msingi ili waweze kuendeleza taaluma yao hiyo.
Dida alizaliwa mwaka 1982, katika Hospitali ya Ocean Road, mjini Dar es Salaam. Alipata elimu ya msingi katika shule ya Ubungo na sekondari ya Makongo, Dar es Salaam. Kidato cha tano na sita alisoma mkoani Tanga na baada ya hapo alijiunga na Chuo cha Uandishi wa Habari cha Dar es Salaam (DSJ). Mwanamama huyo hajaolewa, lakini anaye mtoto mmoja na anaishi Kijitonyama, Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment